(HABARILEO)
HATUA ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe kutaja hadharani
mshahara wa Rais na Waziri Mkuu, imechukua sura mpya baada ya Chama cha
Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE) kulaani hatua hiyo na kuomba
Spika Anne Makinda kuchukua hatua kwa vile ni ukiukaji wa sheria.
Chama hicho kimeeleza kusikitishwa na kitendo hicho kufanywa na
Mbunge aliyehusika na upitishaji wa sheria hiyo huku wabunge wenyewe
wakiwa wakali pale wananchi na wadau mbalimbali wanapohoji mapato yao.
Katibu Mkuu wa Tughe Taifa, Ally Kiwenge alisema Dar es Salaam jana
kwamba pamoja na hatua hiyo kukiuka sheria ya kazi na uhusiano kazini
inayosema mshahara ni siri ya mwajiri na mwajiriwa, pia kitendo hicho si
ajenda ya wafanyakazi hivi sasa.
Alisema ajenda ya wafanyakazi kwa sasa ni kuona wabunge wanapigana
kufa kupona katika kuhakikisha kuwa mshahara wa mfanyakazi unaongezeka
kukidhi mahitaji ya mwezi mzima na kuwaondolea mzigo wa mikopo
inayowaandama.
“Huu si wakati wa wafanyakazi kutaka kujua mishahara ya Rais au
Waziri Mkuu, ajenda yetu kwa sasa ni kuona wabunge wanapigana ili
kuboresha mishahara ya wafanyakazi ili ukidhi mahitaji muhimu tofauti na
sasa,” alisema Kiwenge.
Alisema pamoja na hilo ni mkakati wa wafanyakazi sasa kuona wabunge
wanatumia muda wao uliosalia kabla ya Bunge kuvunjwa kuhakikisha mambo
makubwa mawili yanaingizwa katika Katiba mpya, moja ikiwa ni nafasi ya
mfanyakazi kikatiba ikoje na pia kuona Katiba mpya inasema nini juu ya
hatima ya maslahi ya wafanyakazi.